SPORTS: Zanzibar imekuwa timu ya kwanza kuingia Nusu Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati baada ya sare ya 0-0 na wenyeji, Kenya katika mchezo wa Kundi A jioni ya leo Uwanja wa Kenyatta mjini Machakos, Kenya.
Matokeo hayo yanamaanisha, Zanzibar inafikisha pointi saba baada ya kucheza mechi tatu, ikishinda mbili 3-1 dhidi ya Rwanda na 2-1 dhidi ya Tanzania Bara kabla ya sare ya 0-0 leo na Kenya – na itaingia kwenye mchezo wa mwisho wa kundi lake dhidi ya Libya Desemba 11 kutafuta kulinda rekodi yake ya kutopoteza mechi.
Mapema katika mchezo mwingine wa Kundi A uliotangulia leo mchana, Tanzania Bara ilipoteza nafasi ya kwenda Nusu Fainali baada ya kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Rwanda Uwanja wa Kenyatta pia.
Bara wanakamilisha mechi tatu bila ushindi, wakiwa wamepoteza mbili wakifungwa 2-1 zote dhidi ya Zanzibar na Rwanda baada ya kuanza kwa sare ya 0-0 na Libya na sasa watakamilisha mechi zao kwa kumenyana na Kenya Desemba 11 kabla ya kurejea nyumbani.
No comments:
Post a Comment